Jumanne, 2 Februari 2016

MAHAKAMANI KWA KUPOKEA RUSHWA YA DOLA 3,000



JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
       
  

          





 


MAHAKAMANI KWA KUPOKEA RUSHWA YA DOLA 3,000

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Mkoa wa Kinondoni imemfikisha mahakamani Afisa wa Uhamiaji wa Manispaa ya Kinondoni Bi. Margreth Kokushubira Prosper mnamo tarehe 1/2/2016 kwa kosa la kuomba na kupokea rushwa kinyume na kifungu cha 15(1)(a) cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Namba 11 ya Mwaka 2007. Kesi hiyo Na. 01/2016 iko mbele ya Mhe. Hakimu Obadia Bwegoge.

Bi. Margreth mwenye umri wa miaka 33, alikamatwa tarehe 27/1/2016 katika eneo la kuegesha magari lililopo nje ya jengo la Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni kwa kupokea rushwa ya fedha za kimarekani dola 3,000 kutoka kwa raia wa China Bw. Lizhi Ping. Bi. Margret alikuwa ameomba hongo hiyo kwa raia huyo wa China apate kumrudishia hati kumi za kusafiria za raia wenzake zilizokuwa zikishikiliwa na ofisi ya Uhamiaji ya Wilaya ya Kinondoni. Hati hizo zilikuwa zinashikiliwa na ofisi hiyo kwa ajili ya kuzikagua kufuatia agizo lililotolewa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu Bi. Jenister Mhagama la kuwatambua na kuwakamata raia wa kigeni wanaoishi na kufanya kazi nchini bila kuwa na vibali. Hivi sasa mshtakiwa yuko nje kwa dhamanana kesi yake itatajwa tena tarehe 24/2/2016.

Dola hizo 3,000 alizokamatwa nazo ni sehemu ya dola 6,000 alizokuwa ameomba sawa na fedha za kitanzania shilingi milioni kumi na tatu (13,000,000/-) kutoka kwa Bw. Lizhi Ping.

Mkuu wa TAKUKURU (M) Kinondoni Bw. Benn Lincolin anatoa onyo kwa watumishi wa umma wenye tabia kama ya Bi. Magret Kokushubira Prosper ya kujinufaisha kutokana na maagizo yanayotolewa na viongozi wa Serikali, kuacha tabia hiyo vinginevyo sheria itachukua mkondo wake.



IMETOLEWA NA MKUU WA TAKUKURU (M) KINONDONI

BENN LINCOLIN
2/2/2016

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni

Jumla ya Mara Iliyotazamwa

Kumbukumbu la Blogu